Research Papers

Permanent URI for this collectionhttps://scholar.mzumbe.ac.tz/handle/123456789/1446

Browse

Search Results

Now showing 1 - 3 of 3
  • Thumbnail Image
    Item
    Tija za tohara kwa jamii za Kiafrika: Uchunguzi wa mhusika Omolo katika riwaya ya ua la faraja (2004)
    (Journal of Kiswahili and Other African Languages, 2025) Fuluge, Adria; Duwe, Martina
    Katika jamii nyingi za Kiafrika, tohara ni mchakato wenye thamani na tija kubwa kwa baadhi ya makabila, husuani kwa kijana wa kiume. Katika makabila hayo, asiyetahiriwa huonekana kuwa bado ni mtoto na hajakomaa kifikra na kiutu, ambapo huweza hata kutengwa katika kushirikishwa baadhi ya masuala ya kijamii. Kijana huyo kama umri wake ni mkubwa, huweza kudharauliwa na rika lake na hata waliopo chini yake. Sambamba na hilo, katika maisha halisi ya Waafrika, tohara huchukuliwa kwa thamani inayoweza kuendeleza na kuhifadhi utambulisho wa kitamaduni na kijamii. Kwao, tohara humfanya mtu atambulike kwa namna tofauti na ilivyokuwa awali. Kwa jumla, thamani ya tohara kwa Waafrika ni suala lililowashughulisha wataalamu wengi. Hata hivyo, pamoja na kuwepo kwa tafiti nyingi kuhusu tohara kwa Waafrika, bado tija za tohara kwa kufungamanisha na fasihi andishi haijamakinikiwa kwa umahususi wake. Kwa hiyo, makala hii inashughulikia jambo hilo kwa kumrejelea mhusika Omolo kutoka riwaya ya Ua la Faraja (2004). Data za matokeo haya zilipatikana maktabani kwa kutumia mbinu ya usomaji matini. Vilevile, misingi ya Nadharia ya Sosholojia ya Kifasihi imetumika katika mchakato wa kuchunguza, kuchanganua, na kuwasilisha data zilizozaa matokeo hayo. Mjadala unaonesha kwamba tohara katika maisha ya Waafrika ina tija mbalimbali kulingana na utoshelevu wa kaida zao. Makala hii inajadili tija nne; nazo ni: Kudumisha mila, kuleta heshima kwa mhusika, kujikinga na magonjwa, na kujenga ujasiri na ukakamavu.
  • Thumbnail Image
    Item
    Hatima ya maisha ya Waafrika katika Bunilizi za Kiswahili: Mwegamo wa kifalsafa
    (Ruaha Journal of Arts and Social Sciences (RUJASS), 2021) Duwe, Martina
    Makala hii imefafanua sababu za hatima ya maisha ya mwanadamu kulingana na fikra za Waafrika kwa kurejelea riwaya za Utengano (1980) na Tata za Asumini (1990). Data za msingi zilizofafanuliwa katika makala hii zimepatikana maktabani kwa kutumia mbinu ya usomaji makini. Nadharia ya Udhanaishi imetumika kama mwegamo muhimu katika uchambuzi na mjadala wa data zilizowasilishwa katika katika utafiti uliofanyika. Matokeo yanaonesha kuwa utajiri wa maarifa yaliyomo ndani riwaya teule husawiri maudhui na fikra halisi za Waafrika kulingana na tamaduni zao. Fikra hizo hudhihirisha falsafa inayotawala maisha yao. Pia, hubainisha sababu mbalimbali za hatima ya mwanadamu kulingana na mitazamo ya Waafrika. Kifo ni miongoni mwa sababu zilizobainika wazi katika riwaya teule kuwa kinasababishwa na maamuzi ya Mungu, maovu ya mwanadamu mwenyewe na watu wanaomzunguka katika mazingira yake halisi; na namna Waafrika wanavyofikiri juu ya sababu za hatima ya maisha yao. Mwandishi anayaonesha haya ili kudhihirisha uhalisi wa fikra za jamii yake kama sampuli ya jamii za Kiafrika. Makala hii inahitimisha kuwa fasihi andishi inahifadhi na kuonesha maarifa yanayoisawiri jamii husika.
  • Thumbnail Image
    Item
    Usawiri wa eskatolojia ya Waafrika katika mbolezi za Wangoni
    (CHALUFAKITA 2020, JUZ. NA. 2, 2020) Duwe, Martina
    Eskatolojia ni kipengele kimojawapo kinachodhihirisha falsafa ya jamii za Waafrika kulingana na mila na desturi zao. Tafiti nyingi zilizofanywa kuhusu dhana hii zimejiegemeza katika muktadha wa kiteolojia. Baadhi ya tafiti hizo ni zile zilizofanywa na Baloyi (2008) na Lup (2013). Licha ya kuwapo kwa tafiti hizo, dhana ya eskatolojia ya Waafrika hususani fasihi simulizi za jamii ya Wangoni bado haijamakinikiwa ipasavyo. Aidha, ni wazi kwamba fasihi simulizi ni fasihi inayobeba na kuibua maarifa ya kifalsafa yanayoisawiri jamii husika kulingana na kaida zao. Kwa mantiki hiyo, makala hii inajadili usawiri wa eskatolojia ya Waafrika katika kipera cha mbolezi hususani za jamii ya Wangoni ili kubainisha maarifa yanayobebwa katika kipera hicho. Makala hii ni matokeo ya utafiti uliofanyika kwa kutumia mbinu ya ushuhudiaji shirikishi katika matukio yanayoambatana na suala la kifo na mahojiano ya ana kwa ana na baadhi ya Wangoni katika mazingira yao halisi. Data zimechanganuliwa kwa njia ya maelezo. Data hizo zinaonesha kuwapo kwa eskatolojia ya Waafrika katika mbolezi za jamii hiyo. Hata hivyo, makala hii inajadili vipengele muhimu vitatu tu ambavyo ni: kuamini katika uwepo wa Mungu, mwendelezo wa maisha baada ya kifo na nguvu za waliokufa (mizimu).